Nishati

Mradi wa Kuzalisha Umeme wa Nyerere Katika Mto Rufiji (Stiegler’s Gorge)


Serikali kupitia Wizara ya Nishati imeendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya kimkakati inayolenga kufanikisha utekelezaji wa sera ya viwanda hususani kupitia miradi ya nishati ya umeme.

Serikali imeweka kipaumbele cha kusimamia utekelezaji wa mradi wa kuzalisha umeme wa Nyerere katika Mto Rufiji (Stiegler’s Gorge). Mradi huu ni njia sahihi ya kufikia Uchumi wa Viwanda ifikapo mwaka 2025.

Hafla ya Utiaji saini ya Mkataba wa Ujenzi wa Mradi ilifanyika jijini Dar es Salaam, Tanzania tarehe 12 Desemba, 2018 na kushuhudiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli na Waziri Mkuu wa Misri, Dkt. Mostafa Madbouly. Katika hafla hiyo, Mhe. Rais Magufuli alisisitiza Serikali ya Awamu ya Tano ipo imara na itahakikisha kuwa mradi huo utakaozalisha zaidi ya Megawati 2100 unakamilika kwa wakati ili kuiwezesha Tanzania kuweza kupiga hatua kubwa zaidi katika maendeleo. Pia Rais alisisitiza kuwa Serikali ya Awamu ya Tano imekusudia kuharakisha utekelezaji wa mradi wa umeme wa Nyerere huo kutokana na ukweli kuwa uzalishaji wa umeme kwa chanzo cha maji ni rahisi katika uzalishaji wake ukilinganisha na vyanzo vingine vya uzalishaji wa nishati ya umeme ikiwemo upepo, makaa ya mawe, nyuklia, jua na joto ardhi.

Vilevile, Waziri wa nishati, Mhe. Dkt. Medard Kalemani (Mb) aliongeza kuwa kupitia katika vyanzo mbalimbali vya nishati ya umeme vilivyopo nchini, Serikali ya Awamu ya Tano imekusudia kuhakikisha Tanzania inaweza kuzalisha Megawati 5000 za umeme ifikapo mwaka 2020 na Megawati 10,000 ifikapo mwaka 2025 na hivyo kuiwezesha Nchi kuwa muuzaji wa umeme katika nchi jirani.

Mradi huu unajengwa na mkandarasi wa kampuni ya Arab Contractor kutoka Misri utagharimu kiasi cha Trilioni 6.5 na unatarajiwa kujengwa kwa kipindi cha miezi kati ya 36 mpaka 42 ya ukamilishaji wa mradi huo.

Kukamilika kwa utekelezaji wa mradi wa ujenzi, kutaiwezesha Tanzania kuzalisha kiasi kikubwa cha umeme kitachokasaidia kutekeleza miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo ujenzi wa uchumi wa viwanda na mradi wa reli ya kisasa, hatua itakayoiwezesha kupiga hatua kubwa za maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wake.

Ushiriki wa wananchi

Mpaka sasa mradi umetoa ajira 1151 kati ya hizo 855 ni watanzania na 296 ni wataaalamu wageni kutoka nje .Vijiji saba (7) vimejihusisha na mradi. Mradi unategemea kutoa ajira 6,000 wakati wa ujenzi na wakati wa uendeshaji zitabaki ajira 100. Wakati wa ujenzi kati ya ajira 6000, Asilimia 70 ni za watanzania. Zabuni za makampuni za kusaidia bado hazaijatolewa.

Miradi Mingine ya Umeme

Mradi wa Msongo wa kV 400, North - West

Hatua iliyofikiwa ni:kuendelea na upimaji, na tathmini ya maeneo kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya kupozea umeme vya Kigoma, Mpanda, Sumbawanga, na Tunduma; na kukamilisha taarifa za fidia kwa wananchi watakaopisha mradi Kutoka Kigoma hadi Nyakanazi.

Mradi wa msongo wa kV 400 na Kv 220, North –East Grid ( DarTanga-Arusha)

Hatua iliyofikiwa ni: kukamilisha upimaji na tathimni ya mali za wanachi watakaopisha mradi kwa kipande cha kutoka Kinyerezi-Kiluvya-Chalinze hadi Segera

Mradi wa njia ya kusafirisha Umeme wa Msongo wa Kv 220 ya Geita-Nyakanazi

Hatua iliyofikiwa ni: kufanyika kwa uhakiki wa mali zitakazoathiriwa na mradi; kupatikana kwa mkandarasi atakayejenga njia ya kusafirisha umeme; na kujengwa vituo vya kupoza umeme.

Mradi wa Msongo wa Kv 220 Bulyanhulu - Geita na Geita – Nyakanazi

Hatua iliyofikiwa ni: kukamilika kwa uhakiki wa fidia kwa wananchi watakaopisha mradi pamoja na kuwapata wakandarasi wa utekelezaji wa miradi.


Link za miradi ya umeme: www.tanesco.co.tz